KILIMO BORA CHA UYOGA -sehemu ya 01

                 

Miaka ya karibuni, utaalamu wa kilimo cha uyoga umeanza hapa Tanzania baada ya watu kutilia maanani lishe bora ya protini na manufaa mengine ya zao hilo. Kwa kuwa uyoga upo wa aina mbalimbali, usitawishaji wake hutofautiana katika mahitaji yake, ikiwa ni pamoja na hali ya hewa, malighafi za kuoteshea, urahisi wa teknologia ya kuotesha katika mazingira ya Tanzania na soko lake kwa wananchi na katika hotel. Hata hivyo ni wananchi wachache tu wanaojua kilimo cha uyoga. Uyoga unaozalishwa unafahamika. Aina zinazofaa kwa Tanzania ni zile ambazo hustawi vizuri, kwenye maeneo ya joto la wastani wa nyuzi joto 20C hadi 33C.


Namna Ya Kuotesha Uyoga
Kabla ya kuanza kuzalisha uyoga inabidi kuwa na chumba chenye paa ambalo litazuia jua, mvua, na vumbi. Chumba hiki kinatakiwa kiwe na sakafu inayohifadhi unyevunyevu pamoja na sehemu ya giza ambayo ni muhimu kwa kuotesha utando wa uyoga.

Mbegu za uyoga huzalishwa kwenye maabara zenye vifaa vinavyowezesha kuotesha mbegu hizo bila kuchafuliwa au kuchanganyika na vimelea kama bakteria, ukungu au jamii nyingine za uyoga ambazo haziliwi. Hapa Tanzania hivi sasa maabara hizo zipo Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kituo cha utafiti wa kilimo-Uyolena taasisi ya utafiti wa kilimo cha bustani- Tengeru (HORTI – Tengeru, Arusha).




Hatua Muhimu Katika Kuotesha Uyoga
Hatua muhimu za kuotesha uyoga baada ya kupata mbegu ni kama ifuatavyo:
 

  • Kusanya masalia ya mzao kama vile mabua, majani ya mpunga, ngano, pumba za 
  • mpunga au mahindi, masalia ya miwa baada ya kukamua nk. Vitu hivi hutumika kama mali ghafi kwa kuoteshea uyoga.
  • Mabua, majani ya mpunga au migomba yakatwe kwa urefu usiozidi sm 6, au urefu wa vidole kwa kutumia panga au kisu.
  • Loweka mali ghafi kwenye maji ya kawaida kwa muda wa siku nzima (saa 24).
  • Kisha yachemshe kwa muda wa saa mbili ili kuua vijidudu pamoja na vimelea vilivyomo.
  • Ipua na umwage maji yote halafu tandaza kwenye kichanja kisafi ili yapoe bila kuchafuliwa na vumbi au vijidudu.
  • Kisha jaza mali ghafi hii katika mifuko ya nailoni tayari kwa kupanda mbegu.

Namana ya kupanda
Kuna aina mbili za upandaji:

1. Aina ya kwanza:

 Chukua mfuko wa nailoni wenye upana wa sm 40 - 45 na kimo sm 75. Weka tabaka ya mali ghafi ya kuoteshea yenye kina cha sm 10 katika mfuko halafu tawanya mbegu ya uyoga juu yake.

Baada ya kuweka mbegu, weka tena tabaka nyingine ya vioteshea na kuweka mbegu juu yake. Endelea kuongeza tabaka kwa namna hii mpaka ifike ujazo wa robo tatu ya mfuko.



2.Aina ya pili: 
Changanya malighafi ya kuoteshea (baada ya kuchemshwa na kupoa) na mbegu ya uyoga katika uwiano wa 1: 25 (mbegu : mali ghafi ya kuoteshea) kwa uyoga aina ya mamama (Pleurotus spp.). Kisha mchanganyiko huo ujazwe katika mifuko ya nailoni, mifuko hii iwe na ukubwa wa sm 20 kwa sm sm 40 ambamo unaweza kujaza kilo 1 - 11/2 ya mali ghafi ya kuoteshea. Funga mifuko na toboa matundu kwenye mifuko yenye kipenyo cha sm 1 kwa kila umbali wa sm 6 hadi 10 kwa kila mfuko.



Zingatia: Matundu yawe mengi ili kuingiza hewa ya kutosha ndani ya mifuko. Kumbuka uyoga ni kiumbe hai hivyo unahitaji kupumua.

uotosheaji wa uyoga kwa njia ya mifuko

Matunzo Ya Zao La Uyoga
Weka mifuko kwenye chumba cha giza. Kwa mkulima wa kawaida waweza kutumia kasha lisilopitisha mwanga kama chumba cha giza. Acha mifuko humo kwa muda wa siku 14 - 21 bila kufunua ili ukungu mweupe uweze kutanda vizuri.

Utando wa uyoga ukishatanda vizuri kwenye malighafi ya kuoteshea, hamishia kwenye chumba chenye mwanga na hewa ya kutosha kisicho pigwa na jua. Katika chumba chenye mwanga, mifuko inaweza kuwekwa kwenye, meza, chanja la waya au miti. Mifuko inaweza pia kuning’inizwa kwenye kamba toka kwenye boriti.




Zingatia: Unatakiwa kudumisha hali ya unyevu kwenye chumba hicho cha mwanga kwa kumwaga maji sakafuni. Ukiona vipando vinakauka unaweza kunyunyizia maji yaliyochemshwa na kupoa juu ya mifuko mara tatu au zaidi kwa siku. Tumia bomba la mkononi lenye ukubwa wa lita moja kunyunyizia maji.



Tahadhari: Usizidishe maji kwani maji yakiwa mengi sana yaweza kuozesha uyoga uliyoanza kuota. Aina nyingi za uyoga huanza kutoa vichwa (pini) siku 2 - 3 baada ya kuwekwa kwenye mwanga.

Uvunaji Wa Uyoga

Uyoga huwa tayari kuchumwa siku tatu baada ya vichwa /pini kuonekana. Uyoga uvunwe kwa mkono kwa kushika katikati ya shina la uyoga kisha zungusha hadi uyoga ung’oke. Usiondoe kichwa peke yake katika kuvuna uyoga kwani kubakiza shina huzuia uyoga mwingine kutokea.

ZingatiaMkulima anatakiwa ajue soko la uyoga kabla ya kuvuna ili kuepuka gharama za kuhifadhi. Kwani uyoga ukishavunwa unatakiwa uliwe kabla haujaharibika.


somo hili  litaendelea siku ya kesho 




KILIMO BORA CHA UYOGA -sehemu ya 01 KILIMO BORA CHA UYOGA -sehemu ya 01 Reviewed by BENSON on July 05, 2017 Rating: 5

1 comment

  1. tunashukuru kwa elim ila ningependa kujua soko la huu uyoga nitalipataje?

    ReplyDelete