UFAGAJI WENYE TIJA: ANZA KUFUGA KUKU WATANO UPATE KUKU 200 NDANI YA MIEZI SITA


Related image

Hebu anza na kuku Watano (5) tu Majike  wenye Rika/Umri mmoja (au wanaokaribiana).

Watunze vizuri kwa kuwapatia chakula kilicho  na mchanganyiko kamili wa viini lishe
vinavyotakiwa katika mwili wa kuku,
yaani;

wanga, protini, calcium, chumvichumvi, madini joto nk (kama nilivyoeleza hapa chini). Wawekee na Jogoo mmoja mzuri wa kienyeji/ kizungu/chotara (kama nilivyoeleza hapa chini juu ya uchaguzi wa majogoo).
Wanapoanza kutaga watayarishie mahali pazuri/Kiota kizuri cha kutagia na kuatamia kwa kuwajengea viota ndani ya banda.
Hakikisha mahali hapo hapavuji wala hapapati unyevunyevu wala joto kali sana. Hakikisha mahali hapo pana usalama wa kutosha (mahali wanyama hatari kama vicheche, pakashume, nyoka nk hawawezi kufika).
Kuku wakiendelea kutaga na sasa ukaona wanakaribia kuatamia,Anza kuchagua aina ya mayai unayotaka kuku wako walalie. Hii inamaanisha kuwa; ukichagua mayai makubwamakubwa hayo yanakuwa na vifaranga majogoo na mayai madogomadogo mara nyingi huwa ni ya vifaranga majike.

Acha kuwawekea mayai ya mviringo kama mpira!

Hakikisha kuku wote wanasubiriana ili walalie/ waatamie kwa pamoja.


Weka mayai 12 hadi 15 kwa kila kiota cha kuku 1 kulingana na umbo la kuku wako. 
Kuku anaweza kutaga hadi mayai 30 kwa kila msimu wa kutaga unapofika. Unaweza kutumia mayai machache kati ya 30 kwa kumuatamishia kuku wako huku mayai mengine yakisubiri awamu ya pili ya kuatamiwa.Kwa mfano ukiwawekea kuku wako hao watano, Kuku 5 x Mayai 12 =Mayai 60.

Kwa kawaida kuku huatamia/hulalia mayai kwa siku 19 hadi 21/24 tu hadi anapototoa vifaranga. Hakikisha unawawekea kuku walioatamia chakula chenye viini lishe vya kutosha na maji mengi karibu na viota vyao ili wakitoka kwenye viota vyao wale chakula mara moja na kunywa maji kisha warudi haraka kwenye mayai yao. Hii itasaidia kuangua mayai yote 12/15 bila kuharibu yai hata moja.
Au hata yakiharikbika basi hayataharibika mengi kama ukiacha kuwawekea chakula waende kufukuzana na panzi na vyakula majalalani huko nje na kuchelewa kurudi kwenye mayai yao.
Wakati ukisubiria siku hizo 21/24 anza kujenga kibanda kidogo ndani ya banda kubwa ulilojenga awali au jikoni au andaa boksi kubwa na gumu kwaajili ya kutunzia vifaranga watakaoanguliwa ndani ya siku 21/24 zijazo.
Baada ya kuku hao 5 kuangua vifaranga wako 60 hapo ndipo kazi kubwa ya kulea vifaranga inapoanza. Elewa kuwa ili upate mafanikio haraka hakikisha kuwa kazi ya kulea vifaranga inakuwa yako na siyo ya kuku! Kwanza, Unatakiwa kuondoa na kuchoma moto/kufukia mabaki yote ya mayai na kuboresha usafi wa banda lote ili kuepusha magonjwa kama vile kuharisha, viroboto, papasi nk.
Hapo unaweza kuwatoa vifaranga wako wote 60 mmojammoja kadri wanavyoanguliwa hadi kufikia kifaranga wa mwisho, yaani Yule wa 60 na kuwaweka katika kibanda kidogo/boksi ulichokijenga na kuwawekea mayai mengine mama zao (yale 15/18 kati ya 30 uliyoyabakiza) ili waatamie tena kwa siku 21 hadi 24 zingine.
Unapotoa kifaranga kutoka kwa kuku aliyeatamia humfanya kuku Yule ashindwe kutoka kwenye mayai maana hana mtoto wa kulea.
Akimaliza kuangua mayai yote na ukamuwekea mengine ni rahisi kwake kuendelea kuatamia maana atasubiri kupata vifaranga na ndipo atajikuta amelalia kwa siku 21 zingine bila wasiwasi.
Kwa kufanya hivyo utakuwa tayari umejipatia vifaranga/kuku zaidi ya 100 ndani ya wiki 7 tu! Sasa Unatakiwa kuwajali sana kuku hawa wanaolalia kwa mara ya pili kwa kuwapa chakula cha kutosha, maji, majani ya makongwe, mchicha, mchunga nk ili wapate vitamini na madini mengine muhimu kwa afya zao.
Fanya hivyo hata watakapokuwa wametotoa na ukawanyang’anya vifaranga. Hii itawasaidia ili wasinyonyoke sana manyoya maana kuku wengi hunyonyoka manyoya wanapoatamia. Kwa kufanya hivi, kuku wako watakaa kwa wiki 2 hadi 3 bila vifaranga na kisha wataanza kutaga tena na kuatamia kama mwanzo.


NAMNA YA KULEA VIFARANGA.
Katika ulezi wa vifaranga kama kuku  utawanyang’anya vifaranga vyao utatakiwa kuwajengea banda dogo (ndani ya banda   kubwa/uzio) ili uwawekee chanzo cha joto kama taa/jiko la mkaa (kama ni sehemu/ majira ya baridi).

Kama utatumia jiko la mkaa  unatakiwa kuacha kwanza hadi mkaa mweusi uwake wote ndipo uweke bandani maana  mkaa ukitoa moshi unaweza kuathiri vifaranga vyako.
Angalia namna ya kuweka jiko lako la mkaa juu kidogo ili vifaranga wasiungue. Hakikisha taa yako haitoi moshi sana na  haivujishi mafuta. Pia uwe na akiba ya mafuta ya taa ya kutosha.
Usiweke mafuta mengi kwenye taa maana inaweza kulipuka ikakuletea hasara. Vifaranga wasizidi 50 kwa boksi 1. Hakikisha umewasha taa/jiko lako ndani ya boksi saa tatu au zaidi kabla ya kuwaweka vifaranga ili chumba/boksi lipate joto kabla ya vifaranga kuwasili.
Njia hizi  zinahitaji uangalifu wa hali ya juu sana kwani kuhatarisha/kuua vifaranga ni kuhatarisha maendeleo yako. Kama utaamua kutumia umeme pia ni vizuri zaidi maana inapunguza hatari zaidi.
Kwa hiyoa njia zote tatu unaweza kutumia jedwali lifuatalo ili kuweza kumeneji joto la kibanda cha vifaranga;
UMRI WA KUKU/VIFARANGA JOTO NDANI YA BOX/KIBANDA  CHA KULELEA VIFARANGA JOTO NDANI YA CHUMBA/BANDA
Wiki 1 33-35oc 30-32oc

Wiki 2 30-33oc 27-29oc
Wiki 3 27-31c 24-26oc
Wiki 4 24-29oc 21-23oc
Wiki 5 26-27oc 22-23oc

Baada ya wiki ya 4/5 pasua box/watoe kwenye banda la kulelea ili walelewe kwa joto la kawaida la banda/chumba.
Kwa kawaida joto hupimwa kwa kipimajoto (thermometer), lakini kama huna kipimo hiki, njia rahisi ni kuwaangalia kulingana na tabia zifuatazo;
Kama vifaranga wamejikusanya sehemu moja basi joto ni kidogo bandani mwao, au kama wanaenda mbali na chanzo cha joto huku wanatanua mabawa yao na wakihema harakaharaka basi joto ni kali/  limezidi kiwango.
Pale watakapo tawanyika vizuri ndani ya boksi/kibanda cha kulelea huku wanakula na kunywa maji vizuri basi joto ni la wasta na ndilo linalofaa. Kama unatumia njia ya Boksi, basi unatikiwa kulipanua kulingana na ukuaji na mahitaji ya vifaranga vyako.
Vifaranga wako wape chakula cha vifaranga cha kutosha, maji safi na salama, majani mabichi ambayo hufungwa kwa kuning’inizwa kwa kamba,na CHANJO za minyoo nk ili wapate vitamin, madini na protini itakiwayo na kuzuia tabia ya kudonoana ili wakue vizuri.
Hakikisha kuwa chumba chao ni kisafi na hakina unyevunyevu wakati wote. Unyevunyevu husababisha ugonjwa wa baridi na hufanya vifaranga wajikunyate na kutetemeka na wanaweza kufa ghafla! Inashauriwa kuwa siyo salama kufuga aina nyingine ya ndege kama vile njiwa, bata, bata

mzinga nk kwa kuwachanganya na kuku maana kila aina ya ndege wanamagonjwa yao.

Hivyo kuwachanganya kutakufanya ushindwe namna ya kuwatibu wanapopatwa na ugonjwa.

Pia chawa wa njiwa huleta ugonjwa wa Ndui hasa kuku wanapoangua vifaranga wao.

Hapa ugonjwa unaweza kufyeka vifaranga wako wote 60/100 kama utafuata ushauri wangu!
Baada ya wiki 2 hadi 3 baada ya kuwanyang’anya vifaranga kuku wako wataanza tena kutaga mayai. Wakiatamia wote 5 Kama utaimarisha huduma kwao na kwa vifaranga/kuku wale 100 tayari utakuwa una kuku 105 au zaidi.
Kuku wale 5 wa mwanzo wakiatamia tena kwa siku 21 hadi 48 (kama utafuata mfumo ule wa mwanzo wa kuaatamishia mara 2) utajipatia vifaranga wengine 100 tena na hivyo kuwa na kuku zaidi ya 200 ndani ya miezi 5/6 tu!
Ukiwahudumia vifaranga wale wa mwanzo 100 vizuri kwa miezi 3 na nusu nao wataanza kutaga kama mama zao. kwahiyo, Chukulia  walalie majike 5 wa mwanzo na majike 50 waliopatikana baada ya uzao wa kwanza kwa miezi ile 3 ya mwanzo utakuwa na mitetea 55.
Wote wakiatamia na watoe vifaranga 10 kila mmoja kwa siku zilezile 21 hadi 46, tayari utakuwa na vifaranga 550!
Sasa jumlisha na wale 150 waliobakia kati ya kuku 200 na wote wakakua vizuri utapata kuku na vifaranga zaidi ya 700! Jumlisha na 550 watakaototolewa na mama zao wale 5 wa kwanza na wale 50 wa uzao wa 1 na 2 kwa mara ya 2 si tayari utakuwa na kuku zaidi ya 1,200 ndani ya miezi 6 hadi 8 tu? Hivyo utajikuta unao kuku zaidi ya 1,000!
Kati ya kuku 1,000 ukisema utoe kuku 800 wa kuuza na ukiwauza kwa bei ya Tsh. 4,000 kwa  kila kuku 1 tayari utakuwa na Jumla ya Tsh. 320,000/= ambazo unaweza kufanya mtaji wa mambo mengine au kuboresha mradi wako zaidi. Unafikiri hapo hujaanza kufikia lengo la kuku 1 akuletee shilingi Milioni 1?
Ukiendelea hivi inamaana kuku 1 atakuzalishia zaidi ya hapo.



BANDA LA KUKU.
Unatakiwa kuwa na banda bora la kufugia kuku ambalo litaweza kutunza kuku ili wasiweze kupatwa na madhara mbalimbali kama vile; kuliwa/kujeruhiwa na wanyama wakali, kuchukuliwa na wezi nk.

Lakini banda bora pia litawasaidia kuku kuhimili mabadiliko mbalimbali ya hali ya hewa yanayoweza kujitokeza.
Sehemu ambayo inafaa kwa ujenzi wa banda bora ni ile ambayo inaweza kufikika kwa urahisi, iwe na mwanga wa kutosha, isiwe na upepo mkali na isiyoruhusu maji kusimama au kuingia ndani.
Banda ni vema likawa la ukuta/mbao/ mabanzi.matete/mianzi imara ili lishikilie paa vizuri lisianguke. Kuta hizi zaweza kujengwa kwa matofali ya saruji/matope/kuchomwa/ mabanzi/mbao nk.
Katika kuezeka waweza kutumia mabati/vigae/nyasi. Banda ni vema likawa kubwa kulingana na kiasi cha kuku na umri walionao.
Kitu cha kuzingatia ni kwamba banda liwe na hewa ya kutosha. Kuku wanaofugwa ndani ni vema

wakatengenezewa uzio mpana (angalau Mita 8×10) ili wapate mahali wanapoweza kuota jua,
kupumzikia/kupunga hewa na kufanya mazoezi (wawekee kamba/bembea/ngazi ndani ya banda).

Hakikisha kuwa banda ni imara na  hawatoki nje ya banda na kwenda mbali ili uweze kuwawekea chakula cha kutosha na  maji na hata wale wanaotaga/kuatamia wapate chakula na kurudi haraka.
Banda likiwa kubwa na bora litapunguza magonjwa kwani litakuwa na hewa ya kutosh ambayo itasaidia kupunguza joto na unyevunyevu usio wa lazima bandani mwako. Hii itasaidia uingizaji oksijeni ya kutosha na  kupunguza hewa chafu zenye madhara kwa kuku.
Pia litasaidia namna ya kufanya usafi kwa urahisi na kupunguza vumbi ambalo linaweza kusababisha kikohozi kwa kuku wako. Ni vema banda lisipungue Mita 3 kwenda juu. Mambo muhimu ndani ya Banda.
1. Sakafu nzuri (iliyotengenezwa kwa saruji/ udongo ili isituamishe maji. Isiwe na nyufa ili iweze kusafishwa kwa urahisi.
2. Hakikisha kuwa banda linakuwa na Viota (vitagio) vizuri kwaajili ya kutagia. Viota viwe na urefu wa Sentimita 30 na upana sentimita 30 na kina sentimita 35. Sehemuya mbele izibwe kwa sentimita 10 tu chini. Sehemu zote hizo zizibwe kwa ubao. Kama kuku wako ni wakubwa unaweza kuongeza upana, urefu na kina kiasi cha kutosha mfano, Upana na Urefu 35cm, kina 55cm nk.
Hakikisha kiota/kitagio kinakuwa na giza kiasi maana kuku hupenda kutaga mahala pa giza kidogo/palipojificha. Giza litasaidia kuku asiweze kula mayai au asiweze kudonoana na kuku wengine. Kiota pia kinatakiwa kiwe mahali ambapo ni rahisi kwa kuku kuingia na kutoka, pia iwe ni rahisi kusafisa.
Ndani ya kiota kuwekwe majani makavu/ maranda ya mbao laini na kinyunyize dawa ya unga ya kuzuia viroboto/utitiri kabla ya kuweka nyasi.
AIDHA, ni vizuri sana kuwawekea kuku wanaoatamia mayai wakati wa usiku maana ukimuwekea wakati wa mchana anaweza kuyaacha.
Kuku anayetarajiwa kuatamia ni vema akachunguzwa kama anao utitiri/viroboto/ chawa kwenye manyoya yake. Wadudu hawa humkosesha raha kuku anayeatamia na wengi huacha mayai na kukimbia/wasitulie kwenye viota vyao.
Hali inapelekea kuanguliwa kwa vifaranga wachache. Unaweza kumuona mtaalam wa mifugo kwa ushauri zaidi.
1. Banda liwe na vichanja maana kuku hupenda kulala juu ya vichanja maana nao ni ndege.
2. Vyombo safi na vizuri kwaajili ya chakula na maji.
3. Walazie majani makavu/maranda ya mbao/ makapi ya mazao sakafuni kwa banda zima.


UFAGAJI WENYE TIJA: ANZA KUFUGA KUKU WATANO UPATE KUKU 200 NDANI YA MIEZI SITA UFAGAJI WENYE TIJA: ANZA KUFUGA KUKU WATANO UPATE KUKU 200 NDANI YA MIEZI SITA Reviewed by BENSON on May 20, 2018 Rating: 5

No comments